Tuesday, March 8, 2011

FADHILA ZA HIJAB

 
Imefasiriwa na Salwa Muhammad Mbaaruk


Hijaab ni tendo tiifu kwa Allaah na kwa Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) kasema katika Qur-aan;

{{Haiwi kwa Muumini mwanamume wala Muumini mwanamke kuwa na khiari katika jambo, Mwenyezi Mungu na Mtume Wake wanapokata shauri katika jambo lao. Na mwenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume Wake basi hakika amepotea upotofu ulio wazi.}} Al-Ahzaab: 36

Mwenyeezi Mungu (Subhaanahu wa Ta‘ala) pia kasema;

{{Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao isipokuwa unaodhihirika. Na waangushe shungi zao (juyuubihinna) juu ya vifua vyao}} An-Nuur: 31

Juyuubihinna: Wanachuoni wastahifu kutoka katika zama za as-Salafus Swaalih (watangu wema) wamekhitalifiana kama vazi (Jilbaab) linalofunika mwili lazima lifunike mikono na uso au laa. Leo, wanachuoni wanaoaminika wanasema kuwa mikono na uso lazima ifunikwe. Wanachuoni wengine wanasema bora kwa wanawake kufunika mwili wao mzima.


Hijaab ni ‘Iffah (Stara)
Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) kaifanya Hijaab dhahiri kuwa ni takaso na hayaa. Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) kasema:

{{Ewe Nabii! Waambie wake zako, na binti zako, na wake za Waumini wajiteremshie nguo zao. Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu}} Al-Ahzaab: 59


Katika aya hiyo hapo juu kuna ushahidi kuwa utambulifu wa kuonekana uzuri wa mwanamke ni madhara kwake. Na pindi sababu hiyo ya vile vyenye kusababisha mvuto na vishawishi vitakapoondoka, basi makatazo hayo huondoka. Hii ni kama tunavyoona kwa upande wa wanawake vizee ambao wanaweza kuwa wamepoteza kila kipengele cha kuvutia. Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) kahalalisha kwa wao kuweka pembeni buraa zao na kuonyesha sura na mikono yao, lakini ni bora zaidi kuweka stara zao.


Hijaab ni Twahara (Utakaso)
Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) kautonyesha hekima nyuma ya Sheria ya Hijaab:

{{Na mnapowauliza wakeze haja waulizeni nyuma ya mapazia. Hivyo ndio usafi zaidi kwa nyoyo zenu na nyoyo zao.}} Al-Ahzaab: 53

Hijaab ni muundo wa usafi kwa mioyo ya waumini wa kiume na kike kwa sababu ni kinga au kiziuzi dhidi ya matamanio ya moyo. Bila ya Hijaab, moyo unaweza kutamani mambo machafu. Na hivyo ndio maana moyo upo safi zaidi wakati mwanamke anapojifunika, au kuhifadhiwa (na Hijaab) na vile vile inazuia fitna (matendo maovu). Hijaab inakata taamuli (fikra) mbovu na matamanio mabovu ya moyo.

{{Enyi wake wa Nabii! Nyinyi si kama yeyote katika wanawake wengine. Kama mnamcha Mungu basi msiregeze sauti zenu, akaingia tamaa mwenye maradhi katika moyo wake. Na semeni maneno mema.}} Al-Ahzaab: 32


Hijaab Ni Ngao

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kasema:

Allaah, Aliye juu, ni Pepo, ni Hayii (Mwenye Kustahi), Sittiyr (Kinga). Anapenda Hayaa na Sitr (Kinga)” (Abu Daawuud)


Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) pia kasema:

((Mwanamke yeyote anayevua (hajisitiri sawasawa) nguo zake mbele ya yeyote zaidi ya mume wake (ima kwa kuijionyesha au kusifiwa), amevunja kinga ya Mwenyeezi Mungu juu yake)).


Hadiyth hii inaonyesha namna ambavyo kitendo kinalipwa kutokana na uzuri au ubaya wake.


Hijaab ni Taqwah (Ucha Mungu)

Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anasema:


{{Enyi wanaadamu! Tumekuteremshieni nguo za kuficha tupu zenu, na nguo za pambo. Na nguo za ucha Mungu ndio bora. Hayo ni katika Ishara za Mwenyezi Mungu mpate kukumbuka}} Al-A‘araaf:26


Hizi zama tulizonazo hivi sasa, mtindo mingi ya mavazi iliyopo ulimwenguni leo, ni ya kujionyesha tu na aghlabu sana kuchukuliwa kama ni stara ya mwili wa mwanamke. Lakini kwa wanawake waumini, makusudio ni kujihifadhi miili yao na kuficha maumbo yao. Kama walivyoamrishwa na mwenyewe (Allaah). Na hilo ni tendo la Taqwa (Ucha Mungu).


Hijaab Ni Iymaan


Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Hakuyaeleza maneno yake kuhusu Hijaab ila kwa wanawake Waumini (al-Muuminaat). Katika sehemu nyingi kwenye Qur-aan Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anarejea kutaja "Wanawake Waumini"! Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha), mke wa Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), aliwambia baadhi ya wanawake wa kabila la Banu Tamiym waliokuja kumtembelea yeye (Radhiya Allaahu ‘anha) na wakawa wamevaa nguo nyepesi, yaani nguo ambazo si stara kwa mwanamke wa Kiislam. Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha) akawaambia: “Ikiwa nyinyi ni wanawake Waumini, basi hakika, hilo sio vazi la mwanamke Muuminah analotakiwa kuvaa, na ikiwa sio wanawake Waumini, basi shauri yenu ikiwa mnaona mnafaidika


Hijaab ni Hayaa


Kuna Hadiyth mbili Sahihi ambazo zinasema: “Kila Dini ina maadili na maadili ya Uislamu ni Hayaa” (Ibn ‘Abdil-Barr, al-Mundhiry na kutoka katika kitabu cha at-Targhiyb wa at-Tarhiyb cha Shaykh al-Albaaniy), na “Hayaa ni katika Iymaan na Iymaan imo katika Pepo” (at-Tirmidhy)


Hijaab ni (Ghiyrah) Ghera


Hijaab inaungana na hisia za kimaumbile ya Ghera, ambayo ni lazma kwa mwanamme aliyekuwa hapendi kuona watu wakimwangalia mke na watoto wake wa kike. Ghera ni mtukutiko unaochemka kwa mwanamme unaomsukuma kuona wivu na kuwakinga wanawake waliokuwa wamehusiana nae kutoka kwa wageni na wasio Maharimu zao. Mwanamme mkamilifu wa Kiislamu ana Ghera (wivu) kwa wanawake wote wa Kiislamu kuwakinga hao wanawake na matamanio na uchu wa wanaume. Katika Itikio la matamanio, wanaume wanawaangalia wanawake wengine kwa uchu na matamanio na hawajali kama wanaume wengine wanafanya hayo kwa wake zao na watoto wao wa kike. Mchanganyiko wa kijinsia na kukosekana Hijaab ni jambo lenye kuangamiza Ghera ya wanaume. Uislamu unachukulia Ghera ni sehemu ya Iymaan. Heshima ya mke na binti au mwanamke yeyote wa Kiislamu ni lazima iheshimiwe na kulindwa.

1 comment: